Ibada Lyrics de-musica Ni Magaidi Hasidi, Tuwape Nyekundu Kadi

Ni Magaidi Hasidi, Tuwape Nyekundu Kadi

Tuweze jadiliana,
tukemee ukatili, Natuweze kufaana
waovu tuwakabili, Kwa kupinga zao dhana
Ni magaidi hasidi, tuwape nyekundu kadi.

Wanawalenga vijana, hasa walio mashuleni
Wengi wanapatikana, kwa uwongo mitandaoni.
Tendo zao za laana, tuzizike kaburini
Ni magaidi hasidi, tuwape nyekundu kadi.

Tukiwa mtandaoni,papo hapo ndipo wapo,
Mikakati wamebuni, waliolishwa kiapo,
Vijana tuwe makini, sidanganywe kwa malipo,
Ni magaidi hasidi, tuwape nyekundu kadi.

Mafunzo ya kupotosha, tukatae katakata,
Hitikadi za kutisha,kwetu sije zikakita,
Lango letu wakibisha,mateka atatukamata,
Ni magaidi hasidi, tuwape nyekundu kadi.

Na vyombo vya usalama,twarai mtuhusishe,
Ili kutupa huduma, twawaomba situtishe,
Magaidi kuwazima, sharti mtujumuishe,
Ni magaidi hasidi,tuwape nyekundu kadi.

Wahubiri wahusike,kwa kutoa mwongozo,
Vijana na muafike,kuwe na mazungumzo,
Pamoja tujumuike, tusikubali uozo,
Ni magaidi hasidi, tuwape nyekundu kadi.

Kwa dini wasijibanze, wao sio wanadini,
Waletu na tuwafunze,nyumbani na mashuleni,
Ugaidi wasianze, siingie mashakani,
Ni magaidi hasidi,tuwape nyekundu kadi.

Hili ni letu taifa,tuonyeshe uzalendo,
Wasisababishe nyufa,tuwapinge kwa vishindo,
Tabaki na zetu sifa,kinyoosha yetu mienendo,
Ni magaidi hasidi,tuwape nyekundu kadi.

Usalama uwe mimi,usalama uwe wewe,
Kishikana we na mimi,tafurahia mwishowe,
Tusiseme tu kwa ndimi,tajipatia tu kiwewe,
Ni magaidi hasidi,tuwape nyekundu kadi.

       TUMEMALIZA. 

Hits: 29

Leave a Reply

Your email address will not be published. Required fields are marked *